Wednesday, August 16, 2017

Chadema wadhamiria kurejesha majimbo

By Jesse Mikofu, Mwananchi mwananchipapers@mwananchi.co.tz

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Kanda ya Serengeti kimeanza mikakati ya kurejesha majimbo waliyopoteza katika uchaguzi uliopita wa mwaka 2015.

Majimbo yaliyochukuliwa na CCM katika kanda hiyo yenye Mikoa ya Simiyu, Mara na Shinyanga ni pamoja na jimbo la Musoma mjini (Mara), Maswa, Meatu Mashariki na Magharibi yote ya Mkoa wa Simiyu.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Kanda hiyo, John Heche katika kikao cha viongozi wa chadema kanda hiyo kilichofanyika jijini Mwanza jana.

Heche ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Tarime vijijini amesema katika kikao hicho wamewaagiza viongozi waende kwenye majimbo kukaa vikao vya ndani kuanzia ngazi ya msingi hadi kanda kuweka misingi itakayokiwezesha kushinda kwa kishindo uchaguzi wa Serikali za mitaa mwaka 2019 na Uchaguzi mkuu 2020.


“Tumetoka na maazimio kadhaa, kwanza viongozi wanapotoka hapa kuanzia ngazi za mashina wakafanye vikao vya ndani lengo ni kukomboa majimbo tuliyopokonywa, hiyo ni kwa ajili ya maendeleo kwa mfano ukiangalia halmashauri zinazoongozwa na Chadema zinaongoza kwa miradi ya maendeleo,” amesema Heche

Pia, amewataka wanachama kutokata tamaa kuhusiana na matukio ya kidhalimu yanayondelea ya kuwakamata na kuwaweka ndani viongozi wa chama hicho na kuzuia mikutano ya hadhara ambayo imeruhusiwa kikatiba, badala yake waendelee kupambana mpaka ushindi utapatikana.

Amesema kuna vitisho vingi vinavyotolewa dhidi ya viongozi vikilenga kufifisha demokrasia na nafasi ya watu kushindana kisiasa ili watu waamini CCM kwa nguvu, lakini watapambana navyo bila kuchoka hadi hatua ya mwisho.

“Kuanzia wenyeviti, madiwani na wabunge, wanaokamatwa na kutishwa, tutawalinda na kuendelea kuwapa ushirikiano msaada wowote kisheria hata wanachama wanaotishiwa na kushindwa kufanya kazi zao,” amesema Heche

Mbunge Viti Maalumu Mkoa wa Shinyanga, Salome Makamba amesema kadri serikali inavyozidi kutumia nguvu kubwa kudhibiti kuiminya demokrasia, ndivyo inavyozidi kuwapa nafasi ya kufanya maamuzi magumu na picha mbaya “sio tu kwamba chadema huwa hatushindi, tunashinda ila hatutangazwi.”

Mbunge viti Maalumu Mkoa wa Mara, Catherine Ruge amesema rasilimali kubwa waliyonayo ni nguvu ya umma hivyo watwalinda viongozi wote wanaofanyiwa vitendo vya uzalilishaji kwa kutumia pia msaada wa sheria.

No comments:

Post a Comment