Wednesday, October 11, 2017

SHEHE PONDA AMJULIA HALI TUNDU LISSU NAIROBI , AZUNGUMZIA HALI YA KIUSALAMA NCHINI



Mkutano wa Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu, Sheikh Ponda Issa Ponda na waandishi wa habari, umevamiwa na polisi waliokuwa wanataka kumkamata ili kuzuia mkutano huo usifanyike.

Hata hivyo, polisi hao walioingia katika hoteli ulikofanyika mkutano huo, Kariakoo jijini Dar es Salaam, walishindwa kumpata Sheikh Ponda kwani tayari alikuwa amemaliza kuzungumza na waandishi hao na kuondoka.

Kutokana na hali hiyo, polisi wakawazuia baadhi ya waandishi waliokuwepo eneo hilo na kuwataka kutoa ushirikiano kwa kile kilichozungumzwa na Sheikh Ponda baada ya kumkosa.

Licha ya ushirikiano walioonyesha waandishi hao, polisi waliwakamata waandishi wawili, Ahmed Kombo wa Blog ya Z4 news, na mpiga picha wa gazeti la Daily News, Seleman Mpochi ambaye wakati huo alikuwa anapiga picha katika tukio hilo.

Polisi walimchukua Kombo hadi kituo kikuu cha Polisi na kumtaka awape taarifa iliyoandaliwa na Ponda ambapo alitii na kuwapa ambapo hata hivyo, waliachiwa baadaye.

Pamoja na mambo mengine akiwa katika mkutano huo, amesema Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu amewataka Watanzania waendelee kushikamana ili kuhakikisha wanatetea wananchi na kupinga vitendo vya unyanyasaji vinavyofanywa na serikali ikiwamo kuzuia mikutano ya hadhara kwa wanasiasa.

Amesema amepata faraja kumuona mbunge huyo ambaye anaendelea na matibabu jijini Nairobi, nchini Kenya baada ya kushambuliwa kwa risasi Septemba mwaka huu, kwamba hali yake inaendelea vizuri ambapo pia amemhakikishia kuwa akipona ataendelea na harakati na kutetea maslahi ya wananchi.

“Wakati umefika sasa kila mwananchi, mwanasiasa, viongozi wa dini, haijalishi muislamu au mkristo, wasomi wa vyuo vikuu na watu wa kada mbalimbali tushirikiane pamoja ili kuhakikisha tunakemea vitendo viovu vinavyofanywa kama ni serikali au kikundi cha watu wachache wanaojiita wasiojulikana,” amesema Ponda.

CHANZO : Mtanzania

No comments:

Post a Comment